Masifu ya asubuhi
From Wikipedia, the free encyclopedia
Masifu ya asubuhi ni kipindi muhimu cha Sala ya Kanisa katika madhehebu mbalimbali ya Ukristo, kwa kuwa kinaonyesha kwamba sala ndiyo kazi ya kwanza ya binadamu siku yoyote.
Ni sala rasmi inayofanyika wakati wa jua kupambazuka ili kumtolea Mungu sifa kwa siku mpya inayoanza, ambayo inadokeza pia ufufuko wa Yesu.[1]
Katika utaratibu wa Kanisa la Roma, unaofuatwa na majimbo karibu yote ya Kanisa Katoliki la Kilatini, sehemu kuu za sala hiyo, kati ya utangulizi na baraka ya mwisho, ni utenzi, zaburi moja (au kipande chake) inayotaja asubuhi, wimbo kutoka Agano la Kale, zaburi nyingine ambayo daima ni ya kusifu Mungu, somo fupi au refu kutoka Biblia ya Kikristo, kiitikizano, wimbo wa Zakaria, maombi, Baba Yetu na sala ya kumalizia.
Kati ya sehemu hizo, kilele ni maneno ya Injili (wimbo wa Zakaria na Baba Yetu).